Tuesday, October 9, 2012

Mume ajinyonga kwa kunyimwa unyumba

MKAZI wa Mtaa wa Mpanda Hotel wilayani Mpanda katika Mkoa wa Katavi, Nzego Vicent (33) amejinyonga hadi kufa kwa kutumia kamba ya katani huku akimlalamikia mkewe kwa kumnyima unyumba kwa siku tatu mfululizo bila kupewa sababu zilizomridhisha.

Mashuhuda wakiwemo baadhi ya majirani wa wandoa hao kwa masharti ya kutoandikwa majina yao gazetini, walidai kabla ya kujinyonga, Vicent ambaye alikuwa ametoka kunywa pombe za kienyeji, alifika nyumbani kwake saa 6:20 usiku na kumtaka mkewe ampe unyumba.

Majirani hao walidai kuwa mke wa marehemu, Agnes Nicodemu alilalamikia mumewe kuwa hakuwa tayari kumpatia unyumba kutokana na shughuli alizokuwa amezifanya mchana kutwa na kumsihi avumilie hadi siku itakayofuata kwa kuwa alikuwa amechoka sana.

“Siku mbili mfululizo mama huyo kutokana na kuelemewa na kazi nzito za shamba na nyumbani kwake ambazo alikuwa akizifanya kuanzia alfajiri hadi usiku wa manane, aliendelea kumsihi mumewe ambaye alikuwa akirudi nyumbani usiku kuwa amechoka,“ alidai mama mmoja jirani na wanandoa hao.

Inadaiwa kuwa baada ya Vicent kujibiwa hivyo kwa siku tatu mfululizo hakuridhika na madai hayo ya mkewe ndipo alipoanza kumshutumu kuwa ana uhusiano wa kimapenzi na wanaume wengine.

Inadaiwa siku ya tatu, Vicent alimshambulia mkewe huyo kwa kumpiga sehemu mbalimbali za mwili wake huku akimtolea maneno ya kumtisha kuwa lazima atamuua kwa mapanga iwapo ataendelea kuwa mkaidi katika unyumba.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, Dhahiri Kidavashari, baada ya kuona kipigo kimezidi mwanamke huyo alikimbia nje ili kukwepa kipigo na mumewe naye alitoka nje ya nyumba yao akiwa ameshikilia mashoka mawili na kwenda kusikojuliakana na kuiacha nyumba ikiwa wazi.

Ilipotimu saa 12:30 alfajiri, mwanamke huyo alifuatwa na majirani waliomweleza kuwa mumewe amejinyonga kwa katani jirani na nyumba waliyokuwa wakiishi ndipo alipoandamana nao hadi eneo hilo na kumuona akiwa amening’inia juu ya mti.

No comments:

Post a Comment